ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, October 11, 2017

MVUA YALETA MAAFA RUKWA

KAYA 11 zimebaki bila makazi baada ya mvua kubwa kunyesha na kuezua nyumba katika kijiji cha Matai Asilia, wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa.

Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Isack Sawala, alisema tukio hilo likitokea juzi baada ya mvua kubwa kunyesha ikiambatana na upepo mkali.

Hata hivyo, alisema hakuna mtu aliyefariki dunia kutokana na tukio hilo, lakini baadhi ya watu walijeruhiwa na kupelekwa katika Kituo  cha  Afya  cha Matai  kwa matibabu.

Naye Katibu Tawala wa Wilaya ya Kalambo, Frank Sichalwe, alisema nyumba nane zimebomoka kabisa na hazifai kuishi tena binadamu na wananchi hao wanahitaji msaada wa hali na mali.

Alisema kamati ya maafa ya wilaya inaendelea na jitihada za kuwasaidia wananchi hao ambao wanakabiliwa na hali ngumu kutokana na tukio hilo.

Aidha, alitoa wito kwa wananchi wenye mapenzi mema kutoa misaada ya kibinadamu, ili kuwasaidia wananchi hao kwa kuwa wanahitaji hifadhi kwa ajili yao na mali zao kwa kuwa hawana makazi ya kuishi.

Katika hatua nyingine, alitoa wito kwa wakazi wa wilaya hiyo kuhakikisha wanajenga nyumba kwa kutumia saruji tofauti na sasa kwa kuwa baadhi ya wananchi wamejenga kwa kutumia udongo hali inayosababisha nyumba hizo kutokuwa imara.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.