ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Sunday, June 15, 2025

CCM KUPITISHA WAGOMBEA WENYE UWEZO UCHAGUZI MKUU- GAVU

 Na Mwandishi Wetu


KATIBU wa NEC Oganizesheni na Mafunzo CCM Issa Haji Usi maarufu Gavu amesisitiza Watanzania kuendelea kukiamini Chama cha Mapinduzi kwa kuwa kinaendelea na mipango yake ya kuwaletea Wananchi Maendeleo.

Akizungumza wakati Kongamano la Umoja wa Vijana wa chama hicho UVCCM Wilaya ya Temeke kuelezea utekelezaji wa ilani ya CCM, Gavu amesema kupitia mabadiliko ya Katiba ya chama hicho, yataiwezesha kuisimamia ipasavyo serikali kutekeleza miradi ya kijamii na ile ya kimkakati lengo likiwa ni kuharakisha maendeleo.


Kwa upande wao UVCCM Temeke imekiri kuridhishwa na utekelezaji wa ilani ya CMM 2020/25 huku ukieleza namna Bilioni 900 zilizotolewa ndani ya kipindi cha Serikali ya awamu ya sita ambavyo zimetekeleza changamoto ya madarasa katika vyuo na vyuo vikuu nchini.

Kwa upande wake Zena Mgaya ambaye ni Mwenyekiti wa CCM Temeke amekemea tabia ya baadhi ya vyama vya upinzani kutweza utu na kufanya vitendo ambavyo vina ashiria uvunjifu wa amani.


Wakati huo huo Ofisa Mipango kutoka Manispaa ya Temeke pamoja na Dk.Siriel Mchembe mlezi wa umoja wa vijana wa chama cha mapinduzi vyuo vikuu vya Dar es Salaam wamesema katika miaka minne ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, vyuo vikuu vimenufaika kwa kupata miradi ya ujenzi wa madarasa pamoja na mikopo huku Manispaa ya Temeke ikieleza kupokea zaidi ya Sh.Bilioni 268 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

MAANDALIZI KABAMBE YA JUKWAA LA 4 LA USHIRIKISHWAJI WA WATANZANIA KATIKA SEKTA YA MADINI MWANZA

 NA ALBERT G. SENGO/MWANZA

Katika kuelekea Jukwaa la Nne la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini kutoka Tume ya Madini, CPA. Venance Kasiki, amefafanua umuhimu, malengo na matarajio ya jukwaa hilo litakalofanyika jijini Mwanza kuanzia tarehe 16 hadi 18 Juni, 2025.
CPA. Kasiki amesema lengo kuu la jukwaa hilo ni kutoa fursa kwa Watanzania kushiriki kikamilifu katika uchumi wa madini kupitia huduma na bidhaa wanazoweza kutoa kwenye mnyororo wa thamani ya madini. Ameeleza kuwa, jukwaa hilo pia litaweka mkazo kwenye ushirikiano kati ya serikali, wawekezaji na watoa huduma wa ndani, huku likipambanua fursa mpya zinazopatikana ndani ya sekta hiyo.

Jukwaa hilo litahusisha maonyesho, mijadala ya kitaalamu, mikutano ya kibiashara na majadiliano ya sera ili kuhakikisha Watanzania wanajumuishwa ipasavyo na kunufaika zaidi na utajiri wa rasilimali za madini nchini.






Saturday, June 14, 2025

RAIS SAMIA KUTUA JIJINI MWANZA - RC MTANDA AFUNGUKA JUU YA MAPOKEZI

 NA ALBERT G.SENGO/MWANZA

Mwanza yazidi kung’ara! Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kutua jijini Mwanza kwa ziara ya siku tatu yenye uzinduzi, hotuba na shamrashamra za kiutamaduni. RC Said Mtanda atoa wito: Wananchi, jitokezeni kwa wingi kumlaki Mama Samia – amani, mshikamano na uzalendo ndio silaha yetu!

Friday, June 13, 2025

CRDB Bank Foundation, StartHub Africa zaungana kuwawezesha wanafunzi wa vyuo vikuu

 

Meneja Uendelezaji Biashara Changa wa CRDB Bank Foundation, Sharron Nsule akitoa elimu ya ujasiriamali kwa wanafunzi walioshiriki semina katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Dar es Salaam, Tanzania – June 2025: Katika kuendeleza jitihada za kuinua ujasiriamali na kuwawezesha wanafunzi wabunifu, Taasisi ya CRDB Bank Foundation kwa kushirikiana na StartHub Africa imevitembelea vyuo vikuu vitatu nchini na kutoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa wanafunzi wanaopenda kumiliki biashara baada ya masomo yao.

Ushirikiano huo unaotekelezwa kupitia programu ya “Uni Launch and Scale” tayari umewafikia zaidi ya wanafunzi 1,000 katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Chuo Kikuu cha Iringa na Taasisi ya Uhasibu Arusha (AIA) na kuwapa fursa ya kupata walezi wa kibiashara na mitaji wezeshi kutoka CRDB Bank Foundation.

Akizungumzia mafunzo hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa amesema vyuo hivi vitatu ni mwanzo tu kwani lengo lililopo ni kuwafikia wanafunzi wengi zaidi na kuwawezesha ili wanapohitimu au wakai wanaendelea na masomo yao waanze kushiriki shughuli za kuujenga uchumi baada ya kuwapa elimu ya fedha, mafunzo ya ujasiriamali na uhakika wa kupata mtaji wezeshi.

“Lengo letu ni kuamsha ari ya ujasiriamali iliyomo ndani ya wanafunzi wetu wa vyuo vikuu na kutoa mazingia rafiki kwao kuanzisha biashara zitakazoajiri vijana wenzao badala ya wao wenyewe kuwa waombaji wa kazi wakihitimu. Kupitia ushirikiano huu tunajenga kizazi cha vijana waliowezeshwa kushiriki kuujenga uchumi wa taifa letu,” anasema Tully.

Katika vyuo vitatu ambako wataalamu wa CRDB Bank Foundation na StartHub Africa wamepita, jumla ya biashara 30 zinazomilikiwa na kuendeshwa na wanafunzi zitachaguliwa baada ya kukaguliwa ili kuingizwa kwenye mpango maalumu wa mafunzo ya usimamizi na uendeshaji biashara, utayari wa kifedha na utimamu wa bidhaa.

“Kwa kushirikiana na StartHub Africa pamoja na vyuo vikuu hivi, tunaamini tunaendeleza juhudi za kukuza ubunifu hasa wa kidijitali miongoni mwa wanafunzi wetu hivyo kujenga msingi imara wa biashara zinazoweza kukua na kuwanufaisha wananchi wengi,” amesema Tully.

Programu ya Uni Launch and Scale ambayo CRDB Bank Foundation inashirikiana na StartHub Africa kuitekeleza inalenga kuwawezesha wanafunzi wa vyuo vikuu kutekeleza uwekezaji wanaoukusudia kwa kuwapa mafunzo, ulezi wa kibiashara na uwezeshaji wa mitaji kupitia Programu ya Imbeju iliyojielekeza kuwainua vijana, wanawake na makundi maalumu.

Meneja Programu wa StartHub Africa, Zagaro Emanuel anasema katika ushirikiano huu wanakusudia kuwawezesha vijana wengi wabunifu kupitia mafunzo ya ujasiriamali na elimu ya fedha hivyo kuchangia kuujenga uchumi na kusukuma mbele maendeleo ya Tanzania.

“Tunawahamasisha wanafunzi na wahitimu wa vyuo vikuu, tunawandaa waanzilishi wapya wa biashara watakaosaidia kuleta mapinduzi ya kiuchumi na kuimarisha ujasiriamali nchini kwa kushirikiana na vyuo vikuu, wawekezaji na wawezeshaji. Tukiwa pamoja na Taasisi ya CRDB Bank Foundation, tunaamini tutafika mbali na kuwajumuisha wanafunzi wengi zaidi nchini,” anasema Emanuel.

Meneja huyo anaongeza kwamba programu hiyo inawapa wanafunzi jukwaa la kujitangaza katika soko la ndani, kitaifa na kimataifa na wanapowasilisha mawazo ya miradi yao, wanajiweka kwenye nafasi nzuri zaidi ya kuvutia mitaji huku vyombo vya habari vikiwarahisishia kujulikana kwa biashara zao hivyo kujiongezea umanifu kwa wadau ambalo ni jambo jema kwa kila biashara.

'BOMU LATEGULIWA LIGI KUU' MWENYEKITI AJIUZULU, MTENDAJI MKUU ASIMAMISHWA GHAFLA.

 


Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), Steven Mnguto, amewasilisha barua ya kujiuzulu wadhifa wake, hatua inayokuja wakati ambapo kumekuwepo na mijadala mingi kuhusu mwenendo wa uendeshaji wa ligi hiyo.

Taarifa ya kujiuzulu kwa Mnguto imethibitishwa leo, Ijumaa Juni 13, 2025 na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), likieleza kuwa barua hiyo imepokelewa rasmi na uamuzi huo utazingatiwa kwa mujibu wa taratibu na kanuni za shirikisho hilo.


Katika hatua nyingine, Rais wa TFF, Wallace Karia, amemsimamisha kazi Ofisa Mtendaji Mkuu wa TPLB, Almasi Kasongo, hadi hapo uchunguzi dhidi yake utakapokamilika. Taarifa ya TFF iliyotolewa usiku huu na Katibu Mkuu, Wilfred Kidao, haijaeleza sababu rasmi ya kusimamishwa kwa Kasongo, lakini imesisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mchakato wa kiutawala unaolenga kuboresha uendeshaji wa ligi.


Hatua hizi mbili zimekuja wakati kukiwa na mvutano wa mechi ya watani wa jadi Yanga na Simba ambayo awali ilikuwa ipigwe Machi 8, mwaka huu kabla ya kusogezwa mbele hadi Juni 15 mwaka huu. Hata hivyo wakati kukiwa na mvutano huo huku kila timu ikivutia upande wake, mapema leo bodi ya ligi imetangaza kuwa mchezo huo sasa utapigwa Juni 25.

Ratiba hiyo mpya ya mchezo namba 184 imekuja kufuatia viongozi waandamizi wa timu hizo kukutana na Rais Samia Suluhu Hassan Ikulu jijini Dodoma mapema leo.

KARIAKOO DERBY YASOGEZWA MBELE, KUPIGWA JUNI 25

 


Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imesogeza mbele mechi ya Ligi Kuu namba 184 baina ya Yanga na Simba uliopangwa kuchezwa Juni 15 hadi Juni 25.

Taarifa hiyo imetolewa leo, Ijumaa, Juni 25 na TPLB.

“BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imeusogeza mbele mchezo namba 184 wa
Ligi Kuu ya NBC kati ya klabu ya Yanga na klabu ya Simba ambao ulipangwa kufanyika kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa Juni 15, 2025 kuanzia saa 11:00 jioni.


“Mchezo huo sasa utafanyika Juni 25, 2025 kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa kuanzia saa 11:00 jioni.

“Bodi inazitakia mandalizi mema klabu za Yanga na Simba kuelekea mchezo huo,” imefafanua taarifa ya TPLB.


Taarifa hiyo ya TPLB imetolewa muda mfupi baada ya kusambaa kwa picha zinazomuonyesha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi wa Simba na Yanga, Ikulu Dodoma baada ya kufanya nao mazungumzo.

MOTO WA MAENDELEO MWANZA DUKA JIPYA LAVUTIA UWEKEZAJI MPYA - BIASHARA YAZIDI KUCHACHAMAA

 NA ALBERT GSENGO/MWANZA

Katika hatua inayoashiria kasi ya ukuaji wa sekta ya ujenzi na biashara jijini Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Hassan Masala, ametoa wito kwa wawekezaji hususan wafanyabiashara wa vifaa vya ujenzi kujitokeza na kuwekeza jijini hapa ili kurahisisha upatikanaji wa huduma muhimu kwa wananchi. Akizungumza wakati wa uzinduzi wa duka jipya la vifaa vya ujenzi la ABC Mwanza Hardware, Masala amesema uwepo wa maduka hayo utapunguza utegemezi wa bidhaa kutoka Dar es Salaam umbali wa wa zaidi ya kilimita 1,200 na kupunguza gharama za usafirishaji kwa wananchi wa Mwanza na mikoa jirani. “Tunahitaji makampuni kama haya kuja zaidi Mwanza. Wananchi wetu wanastahili huduma bora, za haraka na zenye bei nafuu. Uwekezaji huu ni dalili ya uhai wa kiuchumi wa jiji letu,” alisema Masala. Kwa upande wake, Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza, Constantine Sima, amesisitiza kuwa ujio wa ABC Mwanza Hardware unamaanisha fursa zaidi kwa Kanda ya Ziwa, huku akilitaja jiji la Mwanza kama kitovu cha biashara kwa mikoa ya kaskazini magharibi. Mwakilishi wa kampuni ya ABC Mwanza Hardware, Bwana Sahares amesema wamejipanga kutoa huduma za kiwango cha juu kwa kutumia teknolojia ya kisasa na kutoa vifaa vya ujenzi kwa bei rafiki, wakilenga kuwahudumia wateja wote wa Kanda ya Ziwa kikamilifu. Mbali na uzinduzi huo, tuangazie pia ni kwa namna gani ujio wa duka hilo jipya la vifaa vya ujenzi utaleta tija kwa wananchi na wafanyabiashara wa jiji la Mwanza. Zulfikar Nanji ni Mkurugenzi wa Kampumi ya Mwanza Huduma, anafafanua kwa kina mafanikio yanayotarajiwa kupitia uwekezaji huu. #samiasuluhuhassan #mwanza

Wednesday, June 11, 2025

UWT KIBAHA MJINI KUNOGILE WAJENGA NYUMBA YA KATIBU NA KUANZISHA MRADI WA MGAHAWA

 


VICTOR MASANGU, KIBAHA

Jumuiya ya  umoja wa wanawake (UWT) Wilaya ya Kibaha mjini katika kuunnga juhudi za Rais awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kutekeleza ilani ya chama kwa vitendo imefanikiwa kuanzisha mradi wa mgahawa ikiwa kama ni moja ya  kitega uchumi kwa ajili ya kuweza kujikwamua kiuchumi  pamoja na mradi wa ujenzi wa  nyumba ya Katibu wa jumuiya hiyo.

Hayo yamebainishwa na Katibu wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Cecilia Ndaru wakati wa kikao cha kikanuni cha baraza hilo ambacho kimeweza kukutana kwa lengo la kujadili masuala mbali mbali ya kimaendeleo, kujiandaa katika kuelekea uchaguzi mkuu, mapokezi ya Mwenyekiti wa UTW Taifa sambamba na kupokea taarifa ya utekelezaji wa ilani ya chama  kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2020 hadi 2025 kutoka kwa madiwani wa viti maalumu.

Katibu Ndaru amesema kwamba lengo lao kubwa ni kuweka mikakati madhubuti ya kuendelea kubuni na kunzisha miradi mipya ambayo itaweza kuwa ni mkombozi mkubwa kwa jumuiya hiyo kuweza kujiongezea kipato pamoja na kuweka misingi imara ya kuweza kuimarisha jumuiya hiyo kuanzia ngazi za chini.

Katika kikao hicho cha baraza ambacho kilifunguliwa  na Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM) Mwalimu Mwajuma Nyamka  ambaye alikuwa mgeni rasmi  amewataka wanawake hao kuhakikisha wanakuwa naa umoja na mshikamano hasa katika kioindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Nyamka katika baraza hilo amewahimiza wanawake kuchangamkia fursa za kugombea nafasi mbali mbali za uongozi ikiwemo katika nafasi ya udiwani pamoja na ubunge na kuwaomba wanampa kura nyingi za kishindo cha hali ya juu  Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan katika uchaguzi huo mkuu  amebainisha kwamba lengo la chama ni kuhakikisha wanashinda katika nafasi zote.

"Nawapongeza sana wanawake wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini kwa kuweza kuchapa kazi kwa bidii na mimi nimefaarijika sana kuona meweza kusimamia vemaa utekelezaji wa ilani ya chama na pia mmeweza kuanzisha mradi wa mgahawa amabo utaweza kuwa ni chachu ya kujikwamua kuchumi sambamba na ujenzi wa nyumba ya katibu kwa hivyo kitu kikubwa mfanye kazi na viongozi ambao bado wapo madarakani achanane na kampeni amabzo hazina faida kwa kipindi hiki,"amebainisha Nyamka.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Elina Mgonja amempongeza kwa dhati Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu kwa kuweza kutenga fedha nyingi ambazo zimekwenda katika kutekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo sekta ya elimu, afya, maji,miundombinu ya barabara pamoja na huduma nyingine za kijamii.

Aidha Mgonja amemshukuru Mbungu wa Jimbo la Kibaha mjini Mhe. Silvestry Koka pamoja na mke wake Mama Selina Koka kwa kuweza kuwa mstari wa mbele kupambana katika kuwasaidia kwa hali na mali kufanikiwa ujenzi wa mradi wa mgahawa pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba ya katibu wa UWT kwa kushirikiana na wadau na viongozi wengine wa chama pamoja na jumuiya zake.


Naye mlezi wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini ambaye pia ni mke wa Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Mama Selina Koka amewahimiza wanawake wote kuwa na umoja na mshikamano hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 na kuwaomba kuwa mstari wa mbele katika kupiga kura lengo ikiwa ni kuweza kushika katika nafasi zote za udiwani, ubunge, pamoja na nafasi ya urais.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka ambaye amefunga rasmi kikao cha baraza hilo ameishukuru kwa dhati jumiya hiyo ya wanawake kwa kuweza kumpa ushirikiano na sapoti kubwa katika kipindi chote ambacho aliingia madarakani na kuahidi kuendelea kushirikiano nao katika masuala mbali mbali ya kimaendeleo na kutatua changamoto ambazo wanakumbana nazo.

Koka amebainisha kwamba tangu aingie madarakani mnamo mwaka 2010 ameweza kuwa bega kwa bega na jumuiya ya UWT ambapo wameweza kushirikiana katika baadhi ya miradi mbali mbali ikiwemo ujenzi wa mradi wa nyumba ya Katibu pamoja naa kiteega uchumi cha mgahawa sambamba na kushirikishwa katika vikao mbali mbali vyebye kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo ikiwemo kutatua kero na changamoto za wananchi.

MKUTANO WA MSEMAJI MKUU WA SERIKALI NA WAANDISHI WA HABARI JIJINI DODOMA.

 Mkutano wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji mkuu wa serikali na waandishi wa habari kutoka Jengo jipya la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo - Mtumba, Dodoma.

Tuesday, June 10, 2025

'RUNGU JINGINE CHADEMA' - MAHAKAMA KUU YAIPIGA STOP KUFANYA SHUGHULI ZA KICHAMA.

 


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimezuiwa kwa siku 14 kufanya shughuli zozote zile za kichama na Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala ndogo ya Dar es Salaam.

Zuio hilo linatokana na kesi namba 8323/2025 iliyofunguliwa na aliyewahi kuwa Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA Zanzibar, Said Issa na wenzake wawili ambayo imetolewa uamuzi leo na Jaji Hamidu Mwanga.

Uamuzi huo umetolewa huku CHADEMA ikikosa muwakilishi wa kisheria baada ya Wakili Jebrah Kambole aliyekuwa akisimamia kesi hiyo kujitoa kabla ya kutolewa uamuzi akidai kutosikilizwa kwa hoja zao.

Hatua ya CHADEMA kuzuiwa kufanya shughuli hizo inatokana na maombi yaliyowasilishwa mahakamani hapo na jopo la Mawakili wa walalamikaji ya kwamba liwekwe zuio hilo hadi kesi ya msingi itakapoanza kusikilizwa Juni 24, 2025.

Mbali na Mohammed, wengine ni Makamu Mwenyekiti Mstaafu wa chama hicho, Ahmed Rashid Khamis na Maulida Anna Komu wanaojitambulisha kama wajumbe wa bodi ya wadhamini.

Katika kesi hiyo ya madai namba 8323 ya mwaka 2025, wadai wanaiomba Mahakama hiyo itamke na kuamuru amri za kutamka kuwa, wadaiwa wamekiuka sheria zinazohusiana na vyama vya siasa na katiba ya chama hicho.

Wamechukua hatua hiyo na kuomba Mahakama iamuru na kutamka hivyo wakidai kumekuwa na mgawanyo usio sawa wa mali za chama na rasilimali za kifedha kati ya Tanzania Zanzibar na Tanzania Bara.

Pia, wanadai kuna ubaguzi wa kidini na kijinsia, pamoja na kutoa maoni na matamko yaliyo na nia ya kuvuruga muungano kati ya pande mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

MWALIMU IKOMBA AMBWAGA LEAH ULAYA URAIS CWT

Mwalimu Suleiman Ikomba.
Mwalimu Suleiman Ikomba.

Hatimaye tambo na majigambo ya wagombea nafasi ya Rais Chama cha Walimu Tanzania (CWT) zimekwisha baada Mwalimu Suleiman Ikomba kutangazwa mshindi akimbwaga kwa mbali aliyekuwa Rais wa chama hicho Mwalimu Leah Ulaya.

Wawili hao walikuwa wamevuta hisia za Walimu na Watanzania kwa ujumla kutokana na nafasi walizokuwa wakizishirikia awali ya mmoja kuwa Rais na Mwingine makamu wa Rais.
 
Tambo za wagombea hao zilisikika mitaani na ndani ya Ukumbi wa Jakaya Kikwete ambao kwa siku tatu ulikuwa na Ulinzi mkali kila kona wa Jeshi la polisi pamoja na Suma JKT.
 
Mwenyekiti wa Kamati ya uchaguzi huo Halima Liveta amemtangaza hayo alfajiri ya leo Suleiman Mathew Ikomba kuwa amepata kura 608 dhidi ya kura 260 alizozipata aliyekuwa Rais wa awamu iliyopita Leah Ulaya wakati kura moja ikiharibika.
 
Hata hivyo, amesema jumla ya wapiga kura walioripoti kwenye uchaguzi huo walikuwa 914 lakini waliopiga kura walikuwa 868.

Mwalimu Leah Ulaya.


MHE. RAIS DKT. SAMIA AKIPOKEA GAWIO NA MICHANGO KUTOKA KWA TAASISI NA MASHIRIKA YA UMMA

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Akishiriki Hafla ya Kupokea Gawio na Michango kutoka kwa Tasisi na Mashirika ya Umma Ikulu Dar es salaam, leo tarehe 10 Juni, 2025.

Monday, June 9, 2025

YANGA BADO WAKO NA MSIMAMO WAO ULE ULE 'HATUCHEZI'


 Uongozi wa Yanga umesisitiza kuwa hautocheza mechi dhidi ya Simba, Juni 15, 2025 kama matakwa yake hayatofanyiwa kazi licha ya leo Juni 9, 2025 kufanya kikao na uongozi wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB).

Taarifa iliyotolewa na Kamati ya Utendaji ya Yanga leo, imesema kuwa msimamo wao hautobadilika kama wanayoyaomba hayatashughulikiwa.

“Uongozi wa Young Africans Sports Club, unapenda kuutarifu umma kuwa, tarehe 7 Juni, 2025 tulipokea barua kutoka Bodi ya Ligi Kuu Tanzania kwa ajili ya kuhudhuria kikao maalum cha kujadili masuala yahusuyo mchezo namba 184 wa Ligi Kuu ya NBC, YANGA dhidi ya Simba.


“Uongozi wa Klabu yetu ulitii wito huo na kushiriki kwenye kikao kilichofanyika leo, Jumatatu Juni 9, 2025 kwenye ofisi za Bodi ya Ligi Tanzania zilizopo jengo la NSSF Mafao House, Dar Es Salaam, kuanzia saa 4:00 asubuhi.

“Baada ya majadiliano ya saa kadhaa, Viongozi wa Klabu waliwasilisha msimamo wa Klabu yetu kuwa hatutashiriki mchezo namba 184 uliopangwa kufanyika tarehe 15 Juni 2025 mpaka pale matakwa yetu tuliyoyawasilisha kwa maandishi kwao yatakapotimizwa.

“Tunawatakia kila la heri Bodi ya Ligi na Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini katika kushughulikia matakwa yetu yenye mustakabali mkubwa

kwenye maendeleo ya mpira wa miguu Tanzania,” imefafanua taarifa hiyo ya Yanga.

Akizungumza mara baada ya mkutano huo na TPLB uliofanyika katika makao makuu ya Bodi, Ilala, Dar es Salaam, Makamu wa Rais wa Yanga, Arafat Haji amesema klabu yao imeshiriki kikao hicho kuwasilisha msimamo wa wanachama na mashabiki wao.


Akizungumzia juu ya kukubali

kucheza mechi dhidi ya Simba Arafat amesema Yanga haikuwahi kusema kama itacheza mechi hiyo.

"Tumemaliza mkutano na tulichofanya ni kuwasilisha msimamo wa klabu kutoka kwa wanachama na mashabiki wetu hilo ndio kubwa," amesema Arafat Mara baada ya kusema hayo, Arafat aliondoka eneo hilo sambamba na viongozi wenzake.

Ofisa Habari wa Bodi ya Ligi Karim Boimanda amesema taarifa kamili juu ya mkutano huo itatolewa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi Almas Kasongo.

Thursday, June 5, 2025

WAZEE BARÀZA LA CCM KIBAHA MJI WAIBUKA NÀ KUTOA TAMKO LA KUMPAMBANIÀ RAIS DKT.SAMIA ASICHAFULIWE KWA MITANDAO

 


VICTOR MASANGU, KIBAHA

 
Baraza la wazee wa chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha mji Mkoa wa Pwani limelaani vikali viendo vya baadhi ya makundi ya vijana kutoka nchini Kenya kutokuwa na busara kwa kuamua kumkosea heshima  Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia kwenye mitandao ya kijamii hali ambayo inaweza kupelekea uchochezi  hali ya sintofamu kwa wananchi.

Wazee  hao wa baraza wametoa maazimioa hayo ya pamoja wakati wa kikao hicho ambacho kimekutana kwa ajili ya kuweza kujadili mambo mbali mbali yakiwemo masuala yanayohusiana na hadhi ya uongozi hasa  kuona Rais wa nchi ya Tanzania Rais Dkt SamiaSulhu Hassan anakosewa heshima na baadhi ya vijana hao wa kenya kitendo ambacho hawawezi kukifumbia macho hata kidogo.

Akisoma maazimio hayo Katibu wa Baraza la wazee wa chama cha  mapinduzi (CCM) ndugu Issack Kalleyya  amebainisha kwamba wameamua kuketi na kutoa maazimio hayo ya pamoja  kutokana na kuwepo kwa mshikamano mkubwa uliopo kati ya nchi ya Tanzania na wenzetu wa nchi za jirani ikiwemo Kenya.

"Kama baraza la wazee wa chama  chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha mjini tumeamua kukutana kwa pamoja na kutoa maazimio yetu juu ya jambo hilo ikiwemo juu ya kuweza kutafakari kwa kina hali ya Amani na utulivu ndani ya Wilaya yetu na nchi kwa ujumla, sambamba na matukio  mbali mbali ambayo yanayoendelea katika nchi jirani ya Kenya ambayo yanafanywa na baadhi ya vijana,"amebainisha Katibu Kalleyya.
 
Aidha katika kikao hicho baraza la wazee limemshukuru kwa dhati  Rais wa  Kenya Mheshimiwa Willian Samoi Ruto kwa maamuzi yake mazuri ambayo ameyatoa ya  kuomba radhi kwa Watanzania na Waganda juu ya matendo ya vijana wao mitandaoni na kwamba  wanathamini sana  hatua yake ya kidiplomasia kama kiongozi wa Kenya katika kutambua umuhimu wa uhusiano mzuri baina ya Taanzania na  nchi  nyingine za jirani.
Kadhalika Katibu wa baraza hilo amesisitiza kuwepo kwa hali ya umoja kwa  Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwa mujibu wa tamko la Mheshimiwa Moses Wetang’ula, Spika wa Bunge la Kenya, ambaye aliyesema kuwa Tanzania haina shida na Kenya na kwamba tunapaswa kuendelea na udugu wetu bila taharuki zisizo kuwa  na msingi yoyote.

Pia kikoa hicho cha baraza katika maazimio yao hawakusita kumsifu na kumpongeza kwa dhati  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan  kwa kuweza kusimamia kwa vitendo utekelezaji wa miradi  mbali mbali ya kimkakati kama vile Reli ya Kisasa (SGR) na Bwawa la Mwalimu Nyerere lililopo Wilayani Rufiji Mkoa wa Pwani , ambapo kutokana na juhudi zake ameiweka Tanzania katika njia ya chachu ya  maendeleo makubwa ya kiuchumi pamoja na  kijamii.

Sambamba na hilo kikao cha baraza hilo kimeweza kutoa  rai kwa Serikali yetu tukufu kulinda heshima ya Taifa letu, kwa kuhakikisha kuwa wageni wote wanaoingia nchini wanazingatia sheria za nchi, ikiwa pamoja na kuwazuia wale wenye nia za kuvuruga  hali ya amani amani ya nchi sambamba na kulaani vikali  matendo ya udhalilishaji dhidi ya Rais  Dkt. Samia Suluhu Hassan ili kuweza kuendelea kudumisha hali  ya amani na utulivu nchini.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa baraza la wazee wa CCM Wilaya ya Kibaha mjini Mtoro Katele amesisitiza na kuweza kutoa wito  kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuchukuwa hatua zinazostahili ili kuhakikisha heshima ya Taifa letu na kuona kwamba inahifadhiwa kwa kiwango kikubwa pamoja  na kuimarisha mshikamano wa hali na mali wa kikanda katika nchi za jirani.

Hivi  karibuni kumekuwepo na baadhi ya vijana kutoka nchini kenya kutokuwa na busara kwa kuanza kukosea heshima Rais wa awamu ya sita Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kupitia mitandao mbali mbali ya kijamii hali mmbayo ilimlazimu Rais wao Willian Samoi Ruto   kuomba radhi kwa Watanzania na Waganda kwa kile ambacho kimefanyika.

MWENGE WA UHURU KUZINDUA KUWEKA MAWE YA MSINGI MIRADI 13 YA MAJI MKOANI TANGA YENYE THAMANI YA BILIONI 16.7

 

 



Na Oscar Assenga, TANGA

JUMLA ya Miradi 13 katika Sekta ya Maji yenye thamani ya Sh.Bilioni 16,713,383,870 inatarajiwa kuzinduliwa na Mbio za Mwenge wa Uhuru 2025 mkoani Tanga ambao unatarajiwa kuwasili mkoani hapa kesho na kuzunguka maeneo mbalimbali kwenye mkoa huo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Meneja wa Ruwasa Mkoa wa Tanga Mhandisi Upendo Omari Lugongo alisema kwamba miradi hiyo itanufaisha wananchi 85,017 ambao wanapata huduma ya maji safi na salama na kuondokana na adha ambazo walikuwa wanazipata awali.

Alisema kila Halmashauri itakuwa na mradi na miradi 6 ya uzinduzi,miradi 5 ya uwekeji mawe ya msingi katika miradi hiyo itakayozinduliwa itajumuisha vijiji 12 lakini kuwahudumia watu 28000 na karibia asilimia 1 ya wakazi wa mkoa wa Tanga.

Alisema kwamba pia kuna miradi ya uzinduzi katika Jiji la Tanga kupitia Tanga Uwasa ambapo kutazinduliwa mita za malipo kabla na ni maelekezo ya Rais Dkt Samia Suluhu ya viongozi wa chama na serikali ili kuhakikisha maji yanatumika kwenye viwango lakini yanatumika wananchi waweze kulipia kulingana na uwezo wao.

Aidha alisema kutakuwa na uzinduzi kwenye Jiji la Tanga ya Mita za malipo kabla 4,000 zitazinduliwa na mwenge pamoja na kuwepo na miradi mengine ya uzinduzi kwenye wilaya za Handeni ,Lushoto ,Mkinga na mwengine utakuwa ni mradi wa uwekeji mawe ya msingi.

Alisema katika wilaya ya Pangani kwenye Jimbo la Waziri wa Maji kutakuwa na mradi wa uwekeji jiwe la msingi mradi wa maji Mkwaja ili uweze kukamilika kwa kipindi kifupi kijacho na katika miradi wanayoweka uzinduzi ni Kwedizinga wilaya ya Handeni Vijiji,Mgombezi Korogwe Mjini na hapo wamejenga visima 900 vya Rais Samia Suluhu.

Aidha alisema kati ya visima hivyo ambavyo ni mradi maalumu wa kutatua changamoto ya maji kwenye maeneo yasiyokuwa na maji wilaya ya Korogwe watakuwa na mradi wa uzinduzi na wilaya ya Muheza watakuwa na mradi wa visima 900 watakwenda kuweka jiwe la msingi lakni watu wameshaanza kupata huduma ya maji ikiwemo wilaya ya Mkinga wanazindua mradi wa maji Gombero na wilaya ya Tanga ambazo ni Mita za Luku za Maji na wilaya ya Lushoto ni mradi wa Funta –Wanga

Meneja huyo alisema pia kuna miradi mitano ya uwekaji wa mawe ya msingi kwenye eneo la Kwamaligwa wilaya ya Kilindi ambao utahudumia vijiji saba na mradi wa Maji kwamahizi ambao utahudumia eneo la Handeni Mjini.

Alieleza pia Mwenge huo utatembelea mradi wa ukarabati miundombinu ya maji Lushoto Mjini ambao utaboresha huduma kwa wakazi zaidi 23,000 na uwekeji jiwe la msingi mradi wa maji Mkwaja na Visima 900 wa Rais kwa wilaya ya Muheza ambapo miradi hiyo yote inakwenda kuwahudumia wakazi wa Tanga asilimia 3 hivyo wanategemea miradi hiyo itakapokamilika itasaidia kuboresha asilimia 3.3 ya wakazi wa Tanga wakati ile asilimia 1 ya miradi itakayozindua nayo inakuwa imeshakamilika.

“Nimpongeze Rais Dkt Samia Suluhu kwa utekelezaji wa miradi hii pamoja na Mkuu wa Mkoa kwa kuendelea kutuongoza vema katika mkoa wetu pamoja na Mwenyekiti wa CCM Mkoa huu Rajab Abdurhaman “Alisema

mwisho

UDSM YAWAITA WADAU WA ELIMU KUSHIRIKI MAADHIMISHO WIKI YA UTAFITI NA UBUNIFU.

 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

CHUO  Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimeutaarifu umma wa Watanzania na kuwaalika wadau wa elimu na maendeleo, kwa ujumla kushiriki katika Maadhimisho ya kumi ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya UDSM yatakayofanyika kuanzia Juni 9- 11, 2025 katika Viwanja ya Maktaba ya Chuo.

Akizungumza na Waandishi  wa Habari Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo-Utafiti, Prof. Nelson Boniface (Pichani) amesema kuwa Maonesho hayo yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 11, 2025 na mazungumzo ya mashirikiano ya kimkakati, kongamano, maonesho na mawasilisho ya watafiti na wabunifu likiwa ni jukwaa la washiriki kupata fursa ya kubadilishana maarifa na ushirikiano.

Aidha, Prof.  Boniface amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo ni: "Kutumia teknolojia ya Dijitali ili kukuza utafiti, ubunifu na ubiasharishaji,".

Ameongeza kuwa miradi mingi itakayooneshwa ni ile ya wanafunzi na Wanataaluma huku akitanabaisha kuwa mtoa Mada Mkuu ni Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), Mhandisi Peter Ulanga na Profesa Lilian Kaale Mkurugenzi katika masuala ya Ubunifu UDSM.

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinatumia fursa hiyo kujipambanua kwa jamii kwa kuonesha shughuli zake za utafiti, ubunifu, huduma kwa umma na ubadilishanaji maarifa kwa kuunga mkono Dira ya  Taifa ya  Maendeleo 2050.



Wednesday, June 4, 2025

UBABE WA TWIGA STARS DHIDI YA DRC MUUAJI NI YULE YULE CLARA LUVANGA

 

TIMU ya taifa ya wanawake ya Tanzania ‘Twiga Stars’ imeibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ‘Léopards Dames’ katika mchezo wa kirafiki leo Uwanja wa Azam Complex Chamazi, Dar es Salaam.


Mabao ya Twiga Stars leo yamefungwa na wacheza wa FC Juárez ya Mexico, mshambuliaji Opah Clement Tukumbuke dakika ya 26, beki Julitha Aminiel Tamuwai Singano dakika ya 43 na kiungo mshambuliaji wa Al Nassr ya Saudi Arabia, , Clara Cleitus Luvanga dakika ya 47, wakati bao pekee la Chui Jike limefungwa na mshambuliaji wa TP Mazembe ya kwao, Lubumbashi Esther Dikisha Bushiri dakika ya 90.


Ulikuwa mchezo wa pili kuzikutanisha timu hizo ndani ya tano, baada ya Ijumaa pia Twiga Stars kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 hapo hapo Azam Complex, mabao ya Twiga Stars yote yakifungwa na Clara Luvanga dakika ya 28 na 88, wakati bao pekee la Léopards Dames lilifungwa na Esther Dikisha dakika ya 72.


Michezo hiyo ni maandalizi ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) kwa timu zote ambazo zinatarajiwa kufanyika nchini Morocco kuanza Julai 5 hadi 26, mwaka huu.


Tanzania imepangwa Kundi C pamoja na Afrika Kusini, Ghana na Mali, wakati DRC ipo Kundi A pamoja na wenyeji, Morocco, Zambia na Senegal na Kundi B kuna Nigeria, Tunisia, Algeria na Botswana.

UKEREWE YAWASHUKURU WAFANYAKAZI BENKI ya CRDB UKARABATI MADARASA MAWILI, MADAWATI 200

 


Mkuu wa Wiliya ya Ukerewe, Mheshimiwa Christopher Emily Ngubiagai amewashukuru wafanyakazi wa Benki ya CRDB kwa kukarabati madarasa mawili na madawati 200 kwa ajili ya Shule ya Msingi Hamkoko.

Akipokea msaada huo kutoka kwa Mkurugenzi wa Rasilimali Watu wa Benki ya CRDB, Godfrey Rutasingwa, mkuu huyo wa wilaya amesea mazingira mabovu ya madarasa yanasababisha utoro kwa watoto wengi jambo ambalo seriklai inashirikiana na wadau kulifanyia kazi ili watoto wote wasome kwa utulivu unaohitajika kufanikisha ndoto zao.

“Hakika leo wafanyakazi wa Benki ya CRDB mmetupa somo kwa kujitoa kwenu kuhakikisha mnaigusa jamii jamii yetu ya wana Ukerewe. Hakika huu ni upendo mkubwa sana kutoka kwa wafanyakazi ambao sio tu inatugusa jamii ya hapa Ukerewe bali Tanzania nzima kwa ujumla. Mmeonyesha kujali na alama hii ya upendo haitosahaulika. Asanteni sana kwa heshima hii kubwa mliyotupa,” amesema Mheshimiwa Ngubiagai.

Amesisitiza kuwa shule zikiwa na miundombinu mizuri huwafanya watoto wapende kusoma kutokana na kuvutiwa na mazingira mazuri na madarasa ya kisasa, madawati bora ya kukalia. Kwa kulitambua hilo, amesema serikali inafanya kila liwezekanalo kuhakikisha inajenga shule mpya popote inapohitajika nchini na kukarabati miundombinu ya hsule za miaka mingi.

Akizungumza na wazazi, walimu na wanafunzi waliokuwepo kwenye hafla ya kukabidhi madarasa na madawati hayo, Mheshimiwa Ngubiagai amesema ni muhimu kwa jamii kujitoa kuchangia kuboresha mazingira ya shule kwa ajili ya watoto wa Kitanzania kujifunza kwa umakini na akaitumia nafasi hiyo kuwapongeza wafanyakazi wa Benki ya CRDB kwa kuonyesha mfano katika kujitoa kwa jamii wanaoyoihudumia na inayowazunguka.

“Hii imekuwa bahati kwetu kwani mngeweza kwenda sehemu nyingine lakini mliona inafaa kuja Ukerewe kusaidia kutatua changamoto za madarasa na kutoa madawati haya 200. Kwa kweli mmetufundisha na kutupa deni kubwa mioyoni mwetu kwani Watanzania wengi huwa wepesi kuchangia harusi na sherehe nyingine ila wazito kujitoa kwenye elimu kama mlivyofanya wafanyakazi wa Benki ya CRDB,” amesema.

Kwa upande wake, Rutasingwa amesema msaada huo umetolewa kupitia Programu ya Employee Volunteering iliyoanzishwa mwaka 2020 ambapo wafanyakazi wa Benki ya CRDB huchanga fedha kutoka kwenye mishahara yao na kuielekeza kutatua kero iliyopo kwenye jamii katika sekta ya elimu, afya, mazingira na watu waishio katika mazingira magumu.

“Moyo huu wa kujitoa kwa wafanyakazi wetu ni mwendelezo wa jitihada zinazofanywa na Benki ya CRDB kurudisha na kuwekeza katika jamii inapotoa huduma. Benki yetu hutenga asilimia moja ya faida yake baada ya kodi kwa ajili ya kuiwezesha jamii. Tunachangia madarasa, madawati, na miundombinu mingine ya shule. tunatoa vifaatiba na kuhamasisha afya ya jamii. Kupitia kampeni ya Pendezesha Tanzania, tunashiriki kutunza mazingira ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na tupo mstari wa mbele katika kuwawezesha wanawake na vijana kujitegemea kiuchumi,” amesema Rutasingwa.

Mkurugenzi huyo amefafanua kuwa utekelezaji wa Programu ya Employee Volunterring unaanzia ngazi ya mfanyakazi mmoja mmoja, matawi, ofisi za kanda mpaka idara za makao makuu ya Benki ya CRDB.

“Katika ngazi ya kanda, tayari tumeratibu na kutekeleza miradi katika kanda za Pwani, Dar es Salaam, na Kaskazini. Leo tunafungua ukurasa mpya wa jitihada hizi katika Kanda hii ya Ziwa kwa kukabidhi rasmi madarasa mawili na madawati 200 kwa shule hii ya Hamukoko hapa wilayani Ukerewe,” ameeleza Rutasingwa.

Kwa wazazi, Rutasingwa amewakumbusha umuhimu wa kuandaa mazingira haya ya kiuchumi kugharimia elimu akieleza kwamb benki ya CRDB inayo Akaunti ya Junior Jumbo inayomwezesha mzazi kuweka fedha taratibu kwa ajili y amahitaji ya mwanaye huku ikimwandaa mtoto kuwajibika kiuchumi kwa kuanza kutumia huduma za benki tangu akiwa mdogo.

“Akaunti hii haina makato na inamwezesha mzazi kuweka akiba kidogo kidogo kwa ajili ya masomo ya mtoto wake, kuanzia elimu ya awali hadi chuo kikuu. Unachohitaji ni cheti cha kuzaliwa cha mtoto, kitambulisho cha mzazi au mlezi, na shilingi 5,000 ya kuanzia ili kufungua akaunti hii,” amesema.

Tuesday, June 3, 2025

CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) MKOA WA MWANZA KATIKA MAANDALIZI YA MAZISHI YA MZEE SILVIN IBENGWE MONGELLA.



Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Mwanza Ndg Michael Masanja Lushinge Smart (MNEC) (katikati aliyesimama) Mapema Leo Tarehe 03, juni 2025 Ameongoza kikao Cha Kamati ya maandalizi ya Mazishi ya Mzee  Silvin Ibengwe Mongella Ambaye ni Baba Mzazi wa Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara Ndg John Mongella Ambacho kimefanyika nyumbani Kwa marehemu Kijiji cha Kabusungu Kata Sangabuye Wilaya ya Ilemela Mkoani Mwanza

Aidha Mwili wa marehemu unatarajiwa kuwasili Uwanja wa ndege Mwanza siku ya Alhamis 05 juni, 2025 majira ya saa 12 Asubuhi na kuhifadhiwa 
Ijumaa 06, juni Mwili wa marehemu utawasili kijiji cha Kabusungu Kata Sangabuye Wilayani Ilemela Kwa Ibaada ya maombolezo kisha Ibaada ya mazishi itafanyika Tarehe 07, juni 2025 katika Kijiji cha Kabusungu

Bwana alitoa na Bwana ametwaa jina lake libarikiwe 

Imetolewa na Ofisi ya Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza


Friday, May 30, 2025

SAMIA: TUSIGWAJIMANISED CHAMA CHETU, MAGWAJIMA TUYAACHE NJE.


Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewataka wajumbe wa chama hicho kuhakikisha mchujo wa wagombea unafanyika kwa haki na weledi ili kulinda hadhi ya chama, akisisitiza kuwa ni muhimu kuepuka kuwapitisha watu wasiostahili.

Akihitimisha Mkutano Mkuu Maalum wa CCM Taifa leo Ijumaa, Mei 30, 2025, jijini Dodoma, Samia amesema chama kisiruhusu kuathiriwa na tabia za baadhi ya watu waliopoteza mwelekeo wa kisiasa.


“Tukitoa mwanya ndugu zangu, tukapitisha wanaotafuta tu, na mie niwemo, ndiyo tunapata wale wanaokwenda huko - chama kinakuwa Gwajimanised,” amesema Rais Samia na kuongeza, “Kwa vyovyote vile tusigwajimanised chama chetu, Magwajima tuyaache nje,”


Amesisitiza umuhimu wa kuwapima wagombea kwa sifa, maadili na uwezo wao, siyo kwa mapenzi binafsi, hofu au mahusiano ya karibu. Aidha, ameonya kuwa mtu ambaye hana uhusiano wa kweli na chama hawezi kusaidia, bali atakivuruga.


“Mcheza ngoma si yake lazima ataharibu... Ukicheza ngoma si yako utaharibu na utajulikana tu,” amesema kwa mafumbo ya kinadharia yaliyolenga kuhimiza uaminifu na ushirikiano wa kweli ndani ya chama.


KUHUSU KATIBA MPYA

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeahidi kuhuisha na kukamilisha mchakato wa Katiba mpya kabla ya mwaka 2030, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani yake ya uchaguzi ya mwaka 2025–2030.


Akizungumza jijini Dodoma leo katika Mkutano Mkuu Maalumu wa CCM, Mwenyekiti wa Kamati ya Ilani ya CCM, Profesa Kitila Mkumbo amesema hatua hiyo inalenga kudumisha demokrasia, utawala bora na mshikamano wa kitaifa.


Amesema CCM inaamini kuwa misingi ya utawala wa sheria, haki za binadamu na demokrasia ni msingi muhimu kwa maendeleo endelevu ya Taifa, na kwamba chama hicho kitaielekeza serikali kuweka mfumo wa kisheria wa kutekeleza falsafa ya uongozi ya 4R. 

Wednesday, May 28, 2025

NIC YATIKISA MIRADI MIKUBWA NCHINI TANZANIA SASA YABISHA HODI MV MWANZA

 NA ALBERT G.SENGO/MWANZA

Kutoka kwenye SGR inayopita kwa kasi, kuelekea kukamilika hadi kwenye daraja la JPM linalounganisha Kigongo na Busisi... na kutoka kwenye nguvu ya maji ya Bwawa la Nyerere hadi kwenye mawimbi ya Ziwa Victoria – NIC haichezi mbali! Sasa, Mfuko wa Bima wa Taifa (NIC) watingisha tena – safari hii wakitua kwa kishindo kwenye meli ya kisasa MV Mwanza! Hiki ni kielelezo cha namna NIC inavyobadilisha si tu taswira ya bima nchini, bali pia maendeleo ya taifa. Hebu tusikie, hatua kwa hatua, jinsi walivyofanikisha yote haya!.

Tuesday, May 27, 2025

'UDHAMINI WENYE TIJA! PAMBA JIJI FC YAVUNA FAIDA KUTOKA NIC'

 NA ALBERT G. SENGO/MWANZA

"Ushirikiano kati ya NIC Insurance na Pamba Jiji FC inayoshiriki Ligi Kuu ya Tanzania Bara, haukuwa tu juu ya udhamini wa jina au kuonekana kwa chapa yetu. Licha ya kupata nafasi kubwa ya kuonekana (visibility) na kueneza brand ya NIC kwa wapenzi wa soka, pia tumeshuhudia matokeo ya moja kwa moja ya kiuchumi. Kupitia uwekezaji wetu kwa timu ya Pamba, tumeweza kuzalisha faida inayokaribia mara tatu ya kile tulichowekeza — hii ni zaidi ya asilimia 300 ya mapato dhidi ya gharama" "Ushirikiano huu unaonyesha jinsi michezo inaweza kuwa jukwaa dhabiti la kibiashara na kijamii." Kauli ya Karim Mesharck Mkurugenzi wa Masoko na mawasiliano NIC Insurance