ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, May 30, 2017

UN: YAFICHUA JINAI NYINGI ZILIZOFANYWA DHIDI YA BINADAMU JAMHURI YA AFRIKA YA KATI.

Umoja wa Mataifa umesema kuna uwezekano jinai dhidi ya binadamu zimefanywa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati.


Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa leo na umoja huo kuhusu Jamhuri ya Afrika ya Kati kuna uwezekano mauaji makubwa, ubakaji, ukataji viungo  na utesaji uliofanywa na pande mbili zilizokuwa zikipigana nchini humo pamoja na makundi ya wabeba silaha kuanzia mwaka 2003 hadi 2015 vikawa ni jinai dhidi ya binadamu.

Katika ripoti hiyo ya Umoja wa Mataifa yenye kurasa 368 iliyotayarishwa na ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa umoja huo yamezingatiwa maelezo yaliyotolewa na watu zaidi ya 1,200 waliotoa ushahidi wao kwa siri na hadharani ili kuyakabidhi kwa maafisa husika kwa ajili ya kuandaa kesi maaalumu za kuwasilishwa kwenye Mahakama Maalumu ya Jinai ya kusikiliza kesi za jinai mbaya zaidi zilizofanywa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Raia waliolazimika kuwa wakimbizi kukimbia mapigano na machafuko Jamhuri ya Afrika ya Kati.


Imeelezwa kuwa lengo la ripoti hiyo ni kujenga matumaini ya kupungua machafuko na vitendo vya ukatili hususan dhidi ya kambi za wakimbizi na wafanyakazi wa utoaji misaada na vilevile kufikisha ujumbe kwa wahusika wa vitendo vya aina hiyo kwamba wajue kuwa kuna nyaraka na ushahidi wa jinai walizofanya, na ukusanyaji wa taarifa zaidi kuhusiana na jinai zao ungali unaendelea.
 
Wimbi jipya la machafuko nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati liliibuka mwaka 2013, baada ya waasi wa Seleka kumuondoa madarakani aliyekuwa rais wa nchi hiyo François Bozizé, huku mgogoro ukishadidi baada ya waasi wa Kikristo wenye kufurutu ada wa Anti-Balaka kuanzisha mauaji ya kutisha dhidi ya jamii ya Waislamu, ambapo maelfu ya watu wameuawa na mamia ya maelfu ya wengine wamekuwa wakimbizi.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.