ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, July 11, 2017

WAZIRI WA ZAMANI WA KENYA NICHOLAS BIWOTT AFARIKI DUNIA.


Nicholas Biwott waziri wa zamani wa Kenya amefariki dunia leo mjini Nairobi wakati alipokuwa akiendelea kupata matibabu.
Nicholas Biwott aliyekuwa waziri katika serikali ya Rais Mstaafu Daniel Arap Moi amefariki dunia katika hospitali moja jijini Nairobi baada ya kuugua kwa muda mrefu.
Biwott aliyejulikana wakati huo akiwa waziri kama 'Total Man" ameaga dunia akiwa na umri wa miaka 77, hayo yameelezwa na msaidizi wake binafsi.
Taarifa zaidi zinasema kuwa, mwendazake Biwott alikuwa akiugua kwa muda mrefu na mara kwa mara alikuwa akilazwa hospitali na hata kuna kipindi aliwahi kuzushiwa kifo. Kwa mujibu wa duru za karibu na familia yake ni kuwa, katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita maradhi yalikuwa yakimzidia mara kwa mara Nicholas Biwott.
Biwott anakumbukwa na wengi katika siasa za Kenya hasa katika kipindi cha utawala wa Rais mstaafu Daniel Arap Moi, ambapo alitambulika kuwa waziri mwenye nguvu katika serikali hiyo.
Biwott alihudumu kama waziri wa masuala ya taifa akisimamia idara za Sayansi na Teknolojia vile vile waziri wa masuala ya ardhi na kilimo cha unyunyizaji.

Mara ya mwisho kuhudumu waziri ilikuwa 2001-2001 ambapo alihudumu kama Waziri wa Biashara, Viwanda  na Utalii wa Afrika Mashariki wakati wa utawala wa Rais Daniel Moi.

Nicholas Biwott (kushoto) enzi za uhai wake akiwa na Rais wa wakati huo wa Kenya Daniel Arap Moi

Aidha Biwott alihudumu kama mbunge wa Keiyo-Marakwet na Keiyo South kwa kipindi cha miaka 28 (1979 – 2007) kabla ya kuwa waziri kwenye utawala wa Rais Mstaafu Daniel Moi. Alianza utumishi wa umma kama mkuu wa wilaya (DO) Meru kati ya mwaka wa 1965 hadi 1966.

Mwanasiasa huyu mkongwe na maarufu ambaye alizaliwa mwaka wa 1940, chama chake cha National Vision Party of Kenya (NVP) kilikuwa kimetangaza kumuunga mkono Rais Uhuru Kenyatta katika uchaguzi ujao. Kifo cha Biwwot kinakuja siku chake tu baada ya Kenya kuondokea na waziri wake wa usalama wa ndani Joseph Nkaissery aliyeaga dunia Jumamosi iliyopita.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.