ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Monday, April 3, 2017

ALIYEKUWA MTENDAJI WA KATA YA BWANGA AFUNGWA JELA MIAKA MITATU (3) KWA KOSA LA KUOMBA RUSHWA


 Mahakama ya Wilaya ya Chato  imemkuta na hatia Aliyekuwa Mtendaji wa kata ya Bwanga Bw. Protase Polycarp Kyakatamba Ambaye ameshitakiwa  kwa makosa mawili ya Kuomba Rushwa ya kiasi cha Tshs. 300,000/= na kupokea Rushwa ya kiasi cha Tshs. 170,000/= kinyume na Kifungu cha 15(1)(a) na (2) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, hukumu hiyo imesomwa na hakimu Mfawidhi wa mahakama ya Wilaya ya Chato Mheshimiwa JOVITH KATO.

Akisoma hukumu hiyo, mbele ya mwendesha mashitaka wa TAKUKURU Bw. AUGUSTINO MTAKI, Mheshimiwa Kato alisema mahakama imemkuta na hatia Mshitakiwa katika makosa yote mawili kama alivyoshitakiwa, na kwamba mahakama imejiridhisha pasipokuwa na shaka lolote na ushahidi uliotolewa na mashahidi wa upande wa Jamhuri kwamba mnamo tarehe 5/2/2016 Mshitakiwa aliomba kiasi cha Tshs. 300,000/= kutoka kwa Bw. Jackson Madereke ili aweze kumwachia Ndugu yake Bw. Kulwa Charles aliyewekwa chini ya ulinzi katika ofisi ya kata ya Bwanga kwa zaidi ya siku Nne, na kwamba mnamo tarehe 6/2/2016 alimtuma Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyarututu Bw. Silvester Nalompa akutane na Bw Jackson Madereke ili aweze kupokea fedha hizo kwa niaba yake ambazo baada ya makubaliano kwa njia ya simu Mtendaji huyo alikubali kupokea kiasi cha Tshs. 170,000/= badala ya Tshs. 300,000/= alizoomba awali.

Baada ya kusomewa hukumu hiyo mshitakiwa alipewa nafasi ya kujitetea kabla ya kutolewa adhabu ambapo mahakama imempa adhabu ya kulipa faini ya Tshs. 500,000/= kwa kosa la kwanza au kifungo jela miaka mitatu (3) na faini ya Tshs. 500,000/= au kifungo cha miaka mitatu (3) jela kwa kosa la pili, na makosa yote yatatumikiwa kwa pamoja.


Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Geita Bw. Thobias Ndaro ametoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Geita kuendelea kuunga mkono TAKUKURU na serikali kwa ujumla katika mapambano dhidi ya Rushwa kwa kutoa taarifa mbalimbali za vitendo vya Rushwa katika ofisi za serikali za mitaa, mahakama na Halmashauri ili watuhumiwa waweze kuchukuliwa hatua za kisheria na hivyo kushiriki kutokomeza vitendo vya Rushwa, Ubadhilifu na Ufisadi katika jamii zetu na hivyo mwananchi atakuwa ameshiriki kukata mnyororo wa Rushwa. 

IMEANDALIWA NA MADUKA ONLINE

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.