ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, July 20, 2018

AMNESTY WAPINGA HUKUMU YA KIFO KWA MISS MAGEREZA.



Shirika la Amnesty International limetoa wito wa kubatilishwa kwa hukumu ya kifo iliyotolewa dhidi ya malkia wa urembo gerezani nchini Kenya Ruth Kamande.

Mwanamke huyo alihukumiwa kifo Alhamisi baada ya kupatikana na kosa la kumuua mpenzi wake miaka mitatu iliyopita katika mtaa wa Buruburu, Nairobi.

Bi Kamande, 25, amekuwa akizuiliwa rumande katika gereza kuu la wanawake la Lang'ata jijini Nairobi ambapo mwaka 2016 aliibuka kuwa malkia wa shindano la urembo lililoandaliwa humo gerezani.

Mkurugenzi mkuu wa Amnesty International nchini Kenya Irungu Houghton amesema mwanamke huyo anafaa kusaidiwa kujirekebisha badala kuhukumiwa kifo.

"Tunasikitika kwamba Kenya inaendelea kutoa adhabu hii katili, isiyo na utu na iliyopitwa na wakati. Hukumu hii ni pigo kwa rekodi nzuri ya Kenya ya kuendelea kubadilisha hukumu za kifo kuwa hukumu za vifungo jela," amesema.

"Hakuna ushahidi wowote wa kuaminika kwamba hukumu ya kifo huwazuia watu kutekeleza uhalifu zaidi ya adhabu za aina nyingine. Hukumu hii ya kifo inafaa kubatilishwa mara moja na Ruth Kamande asaidiwe kurekebisha tabia."

Ingawa huku ya kifo huendelea kutolewa kwa makosa ya mauaji na wizi wa kutumia mabavu nchini Kenya, haijatekelezwa kwa mfungwa yeyote nchini Kenya katika kipindi cha miaka 30.

Rais Uhuru Kenyatta na mtangulizi wake Mwai Kibaki walibadilisha hukumu ya wafungwa wengi waliokuwa wamehukumiwa kunyongwa katika kipindi cha miaka kumi iliyopita na kuwa vifungo vya maisha jela.

Wafungwa takriban 6,747 wamenufaika kupitia hatua hiyo.


Hukumu ya kifo iliondolewa katika mataifa 139 duniani lakini bado kuna nchi zinazotekeleza hukumu hiyo zikiwemo Marekani, China, Pakistan na Saudi Arabia.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.