ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, May 2, 2018

SHAMBULIZI DHIDI YA MAKAO MAKUU YA TUME YA UCHAGUZI LIBYA LAUA 12.

Shambulizi dhidi ya makao makuu ya Tume ya Uchaguzi Libya laua 12
Kwa akali watu 12 wameuawa baada ya kundi la kigaidi kushambulia kwa mabomu na risasi makao makuu ya Tume ya Uchaguzi nchini Libya leo Jumatano.
CHANZO/PARStODAY
Khaled Omar, msemaji wa tume hiyo ambaye ameponea chupuchupu kwenye hujuma hiyo amesema magaidi kadhaa waliokuwa wamejifunga mabomu waliingia katika ofisi za tume hiyo na kujiripua huku wenzao wakifyatua risasi ovyo dhidi ya maafisa wa tume hiyo.
Amesema maafisa watatu wa tume hiyo na wanne wa usalama ni miongoni mwa watu waliouawa kwenye shambulizi hilo lililofanyika katika mji mkuu Tripoli.


Maafisa usalama nchini Libya

Hadi tunaenda mitamboni, hakuna kundi lililokuwa limetangaza kuhusika na hujuma hiyo, ingawaje kundi la kigaidi na ukufurishaji la Daesh (ISIS) limekuwa likifanya mashambulizi ya aina hii katika nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika.
Mwezi uliopita, Ghassan Salamé, Mjumbe wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Libya alionya kuwa, licha ya kwamba ni jambo la dharura kuhakikisha uchaguzi unafanyika nchini Libya kabla ya kumalizika mwaka huu wa 2018, lakini pamoja na hayo kuna hatari uchaguzi huo ukazidisha matatizo ya kiusalama ya Libya badala ya kuyatatua.
Alisisitiza kuwa, kufanyika uchaguzi wa rais nchini Libya bila ya kuweko Katiba inayokubaliwa na pande zote hasimu, ni jambo gumu sana. 
Uchaguzi wa bunge ndio uliokuwa wa mwisho kufanyika nchini Libya mwaka 2014 na matokeo ya uchaguzi huo ni kuzuka mzozo mkubwa uliopelekea nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika kuwa na mabunge mawili na serikali mbili tofauti.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.