ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, September 16, 2017

VITUO VYA AFYA 172 KUKARABATIWA NA UBALOZI WA CANADA.



Jaffo-  “Mabilioni  Kwa Afya za Watanzania”
Na. Atley Kuni- TAMISEMI
Serikali imepanga kukarabati vituo vya afya 172 kutokana na fedha kutoka Benki ya Dunia na Ubalozi wa Canada ambapo wametoa jumla ya Dolla za Kimarekani Mil 88 sambamba na Bil.12 fedha za kitanzania zilizovuka katika mwaka wa fedha wa 2016/2017.

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mh. Seleman Jafo (Mb) amesema lengo la serikali nikuhakikisha ifikapo Desemba 30, 2017 shughuli hiyo iwe imekamilika ipasavyo kwa kusimamiwa karibu na Waheshimwa Wakuu wa mikoa wakisaidiana na Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya.

Jafo amesema kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Serikali imepokea Dolla za kimarekani  Mil. 66 kutoka Benki ya Dunia ambapo vituo 103 vitakarabatiwa aidha pia Serikali  kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI, imepata Msaada kutoka Ubalozi wa Canada wa dolla za kimarekani Mil 22, ambapo vituo 44 vya afya vitakarabatiwa kwa fedha hizo. 

Naibu waziri huyo alisema,  fedha zingine zitakazo tumika katika zoezi hilo ni zile zilizo vuka katika mwaka wa fedha uliopita.

“Vituo 25 vitafanyiwa ukarabati kupitia fedha za Benki ya Dunia na mfuko wa afya wa pamoja zilizovuka mwaka wa 2016/2017, ambapo Bil.12 za kitanzania zitatumika,” alisema Jafo na kuongeza  kwamba kila  “kituo kitapatiwa shilingi Mil. 500 za kitanzania na baada ya ukarabati serikali itakuwa na jukumu lakupeka vifaa katika maeneo hayo”.

Waziri Jafo amesema, Maeneo ya kipaumbele wakati wa ukarabati huo ni pamoja na  Upasuaji (Theater), Wodi za mama na Mtoto (Martenity), Maabara(Laboratory), pamja na Nyumba za watumishi sambamba na maeneo mengine ya kipaumbele kutokana na fedha zilizopo.

Katika hatua nyingine Jafo amewagiza Makatibu Tawala wa mikoa kuwasilisha Taarifa ya kila mwezi ofisini kwake juu ya maendeleo ya ukarabati, huku akiwataka Wakurugenzi na watendaji wengine kusimamia kwa ufasaha zoezi hilo. 

Naibu Waziri hakusita kuonya juu wale wote watakao kwenda kinyume na maagizo na maelekezo ya serikali yaliyotolewa.

“Nawaomba Wah. Wabunge na Madiwani kushirikiana bega kwa bega na watendaji katika kufanikisha zoezi hili kwa ufanisi, alisema Jafo na kuongeza kwamba,  “ofisi yangu haita mvumilia Kiongozi au Mtendaji yeyote atakaye onekana kutumia fedha hizo vibaya au kushindwa kutimiza wajibu wake na kisha kukwamisha shughuli hii muhimu yenye nia njema kwa maisha ya watanzania.

Akihitimisha maagizo hayo  Naibu waziri Suleima Jafo, amezishukuru  Wizara zote za kisekta katika kusukuma gurudumu la maendeleo  na kwenda sambamba na kasi ya Rais  Mh. Dkt. John Pombe Magufuli ya HAPA KAZI TU,  ikiwapo, Wizara ya Afya, Fedha na Mipango pamoja na watendaji wa Ofisi yake ambao walikuwa bega kwa bega katika mchakato wote wa kupatikana kwa fedha.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.