ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Monday, June 19, 2017

WATETEZI WATATU KULITETEA GAZETI LA MAWIO.

BARAZA la Habari (MCT), Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC) na Umoja wa Vilabu vya Habari Tanzania (UTPC) vinakusudia kufungua kesi kwenye mahakama kupinga uamuzi wa serikali wa kulifunga gazeti la Mawio.

Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ilitangaza kulifunga gazeti hilo kwa miezi 24 kuanzia Alhamisi iliyopita, kwa kuchapisha taarifa zinazowahusisha marais wastaafu Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete kwenye sakata la mikataba mibovu ya madini.

Wakizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, wadau hao walisema hawajaridhika na hatua zilizochukuliwa na serikali katika kulifunga gazeti hilo kwa sababu ni kinyume cha mabadiliko ya Sheria ya Huduma ya Habari ya mwaka 2016.

Kaimu Katibu Mtendaji wa MCT, Pili Mtambalike, alisema kimsingi sheria hiyo haimpi waziri mamlaka ya kutoa adhabu kama aliyoitoa dhidi ya gazeti hilo.

Alisema hatua iliyochukuliwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe, inalenga kuvinyima uhuru vyombo vya habari nchini.

Mtambalike alisema ni vema serikali kupitia Waziri Mwakyembe ikakaa chini na kutafakari upya na pia kufanya mazungumzo na uongozi wa gazeti hilo ili kutengua adhabu aliyoitoa.

"Serikali itengue uamuzi wake wa kulifungia gazeti la Mawio kwani unaenda kinyume cha Katiba pamoja na Sheria ya Huduma ya Habari ya mwaka 2016 kwa kuwa haimpi waziri mamlaka ya kutoa adhabu kama hiyo," alisema.Alisema zaidi: "Kwa sababu hakuna sehemu ya kupeleka rufani dhidi ya uamuzi wa waziri katika Sheria ya Huduma za Habari, endapo hakutakuwa na mazungumzo kati ya gazeti husika na waziri, sisi tutakwenda mahakamani kwa kushirikiano na Mawio kuonyesha haki zilizokiukwa juu ya hatua hiyo.

"Ikumbukwe kwamba vyombo vya habari, yakiwamo magazeti, hufanya shughuli zao kwa mujibu wa sheria na Katiba inasema wazi chini ya ibara ya 18 kwamba Watanzania wote wana haki ya kutafuta, kupokea na kutoa habari na maoni kwa njia yoyote, hivyo kwa mujibu wa sheria na vipengele hivyo vya Katiba, serikali inapaswa kuondoa marufuku yake dhidi ya gazeti la Mawio."

Naye Mkurugenzi wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, alisema sehemu ya sheria ambayo waziri alitumia kulifunga gazeti hilo haina uhusiano na sehemu ambayo imewekwa kosa.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.