ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, June 22, 2017

TAMKO LA CCM KUFUATIA KUCHOMWA MOTO NYUMBA YA MWENYEKITI.

Hai. Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilayani Hai, kimevalia njuga sakata la kuchomwa moto nyumba ya mwenyekiti wa chama hicho wilaya hapa, Dk Amin Uronu kikitaka Serikali na vyombo vya ulinzi kuchukua hatua haraka kwa atakayebainika kutenda kosa hilo.

Tamko lililotolewa jana na Katibu wa CCM Wilaya ya Hai, Kumotola Kumotola limesema hawako tayari kuendelea kuvumilia matendo ya aina hiyo yanayowakosesha amani wanachama wake.

“Kamati ya siasa ya halmashauri kuu inalaani kitendo hicho na vitendo vingine vyote vinavyoashiria uvunjifu wa amani na kusababisha taharuki kwa wanachama, wananchi na wapenzi wote wa familia ya CCM wilayani Hai,” alisema Kumotola.

Dk Uronu alinusurika kifo akiwa na familia yake Juni 19, baada ya nyumba yake kuchomwa moto na watu wasiojulikana usiku wa manane katika Kijiji cha Nshara, Machame wilayani Hai.

Katika tamko la CCM, imetaka uchunguzi kuhusu tukio hilo ufanyike kwa kina ili kubaini chanzo.

Pia, chama hicho kimeiomba familia na wananchi kuwa watulivu katika kipindi ambacho vyombo vya ulinzi na usalama vinahangaikia kujua ukweli wa jambo hilo.

Kutokana na hali iliyojitokeza, CCM imewaomba wanachama na wananchi wa Kata ya Machame Kaskazini, kutoa ushirikiano wa dhati kwa vyombo vya ulinzi na usalama ili waliofanya kitendo hicho wabainike haraka.

Juzi, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Hamisi Issah alisema tukio hilo limemsababishia majeraha makubwa mwenyekiti huyo ambaye bado amelazwa katika Hospitali Teule ya Misheni ya St Joseph iliyopo Moshi mjini.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.