ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, November 15, 2016

UGENI WA NORDIC WATUA WIZARA MAMBO YA KATIBA NA SHERIA KUANGALIA UTEKELEZAJI WA MIRADI MBALIMBALI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome akitoa neno la ukaribisho kwa ujumbe kutoka nchi za Nordic ulipotembelea wizara wake jana 14/11/2016 jijini Dar Es Salaam.(Picha na Zainul Mzige wa Modewjiblog)

Serikali ya Tanzania imeshukuru msaada mkubwa unaotolewa na Mashirika ya Umoja wa Mataifa katika kuhakikisha kwamba taifa linakuwa na mfumo imara wa utoaji haki kwa kuzingatia demokrasia na uwajibikaji.

Serikali imesema kumekuwepo na mabadiliko makubwa katika mfumo ya utoaji haki nchini kutokana na misaada iliyotolewa na nchi hizo kupitia Mashirika ya Umoja wa Mataifa ambao unasaidia mpango huo wa UNDAP.

Hayo yameelezwa wakati ujumbe mzito wa kutoka nchi za Nordic ulipotembelea Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria. Nchi hizo za Nordic pamoja kutoa mchango wake mkubwa katika bajeti za serikali ya Tanzania pia hutoa mchango mkubwa kwa mashirika ya Umoja wa Mataifa yanayofanya shughuli zake nchini.

Mataifa hayo ni ya Sweden, Norway, Denmark, Finland na Iceland ambayo kwa pamoja yanaitwa mataifa ya Nordic ni wadau muhimu wa Umoja wa Mataifa na pia kwa serikali ya Tanzania.

Ujumbe kutoka nchi hizo upo nchini kwa ajili ya kuimarisha mahusiano kati yao na Mashrika ya Umoja wa Mataifa yanayofanyakazi kama taasisi moja na nchi hizo (Delivering as one) kwa lengo la kuimarisha na kusukuma mbele malengo ya maendeleo endelevu (SDGs).

Katika ziara hiyo iliyoanzia Novemba 14 wajumbe hao waliweza kuangalia utekelezaji mbalimbali wa miradi ya Umoja wa Mataifa na hasa hatua za mwanzo za miradi ya UNDAP ll.

Ujumbe huo wenye watu 13 kutoka Wizara za Mambo ya Nje za mataifa hayo wanatarajia kuzuru pia Kigoma na Dodoma wakimaliza Dar es Salaam.

Wakiwa Dar es Salaam, jana na leo watakutana na wawakilishi wa taasisi mbalimbali zisizo za kiserikali na AZAKI na pia wanatarajia kutembelea ofisi za Bunge.Taarifa iliyotolewa katika mkutano huo imesema ingawa msaada wa Umoja wa Mataifa umekuwa siku zote ukililenga eneo maalumu linaloshughulikiwa na mashirika tofauti ya Umoja wa Mataifa, imekuwa nguvu kupima athari zake katika maeneo mbalimbali yaliyokusudiwa.
Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Awa Dabo akielezea dhumuni la ziara ya ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana na wataalam kutoka Umoja wa Mataifa ulipotembelea wizara hiyo jana 14/11/2016 jijini Dar Es Salaam. 

Hata hivyo imeelezwa kuwa kupitia programu mbalimbali na miradi katika demokrasia na uwajibikaji kuwezesha utawala bora, kumefanya kuwepo na nafuu fulani.

Serikali ya Tanzania ilielezea matumaini yake kwamba UNDAP ll, Mashirika ya Umoja wa Mataifa yakifanya kazi kama taasisi moja yatasaidia wizara katika kufanikisha kwa namna sahihi mfumo wa haki kwa wananchi.

Programu hizo ni pamoja na UNDAP 1 iliyosaidia wizara kutengeneza na kutekeleza mpango wa haki za binadamu (MHRAP 2013-2017). Mpango huo ulibainisha maeneo mbalimbali yaliyotakiwa kufanyiwa kazi na wadau mbalimbali.

UNDAP I ilisaidia wizara kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa serikali kujenga uwezo kwa wafanyakazi wake katika masuala ya majadiliano katika mikataba na namna ya kuiandika hasa katika sekta ya uziduaji.
Mkurugenzi Idara ya Katiba na Ufuatiliaji Haki Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria Bw. Patience Ntwina (aliyesimama) akitoa taarifa ya utekelezaji wa miradi mbalimbali inayofadhiliwa na Umoja wa Mataifa kwa ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana na wataalam kutoka Umoja wa Mataifa ulipotembelea wizara hiyo jana 14/11/2016 jijini Dar Es Salaam. 

Wanasheria kadha wa serikali na majaji walinufaika na elimu hiyo.

Aidha chini ya UNDAP I, Umoja wa Mataifa ulitoa msaada wa kiufundi kwa wizara kwa lengo la kuwezesha kufanya utafiti kuhusu hali ya mfumo wa haki wa mtoto nchini Tanzania na kuweza mkakati endelevu wa haki za mtoto kuanzia wmaka 2013-2017.

Wizara pia inasaidiwa kufuatilia mkakati huo kupitia majukwaa ya haki za watoto yanayofanyika kila mwaka.

Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria kwa mujibu wa sera ndiyo iliyokabidhiwa majukumu ya kutengeneza kanuni na viwango, kuratibu na kufuatilia utii usio na shuruti katika mfumo wa sheria na hivyo kupata matokeo yaliyokusudiwa ya sheria husika.

Wizara hii inajishughulisha na masuala ya Katiba, utawala na utoaji wa haki; uandishi wa sheria; uendeshaji wa mashtaka; Mikataba na sheria za kimataifa: msaada wa kisheria na haki za binadamu;usajili uboreshaji wa sheria, kabidhi wasihi, udhamini na mufilisi na kadhalika
Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Mdemu akizungumzia ufadhili wa Umoja wa Mataifa kwa ofisi yake wakati wa mkutano na ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana na wataalam kutoka Umoja wa Mataifa uliofanyika katika Wizara ya Mambo ya Sheria na Katiba jana 14/11/2016 jijini Dar Es Salaam. 

Mamlaka ya Wizara katika mambo mengi ni mtambuka na hivyo kuifanya kuwa na ugumu fulani katika utendaji wake.

Aidha akifafanua zaidi amesema kutokana na misaada ya mashirika ya Umoja wa Mataifa, Watanzania wameweza kuwa na mfumo bora zaidi wa haki kwa watoto wanaoingia matatani na sheria.

Aidha watoto zaidi ya 1,500 wamepatiwa msaada wa kisheria katika mji wa Mbeya na Dar es Salaam na yote hayo yamewezeshwa na UNDAP l.

Wizara pia iliangalia matatizo ya ukatili wa kijinsia na watoto katika Dar es Salaam, Dodoma na Kilimanjaro na matokeo yake kusambazwa kwa wadau mbalimbali kwa kuyafanyia kazi.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nchi Afisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Zanzibar Bw. Kubingwa Mashaka Simba akitoa taarifa ya utekelezwaji wa miradi inayofadhiliwa na Umoja wa Mataifa kwa ujumbe wa wataalam wa Umoja huo waliotembelea Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria Tanzania Bara jana 14/11/2016 jijini Dar Es Salaam. 

Aidha kwa kusaidiwa na Umoja wa Mataifa ambayo iliratibu mkutano wa kwanza wa wadau kuzungumzia sheria ya ndoa ya mwaka 1971 katika hali ya kuongeza haki zaidi ka wanawake na watoto.

Pia alisema katika UNDAPll mashirika hayo ya Umoja wa Mataifa yanasaidia pia kuangalia mfumo wa haki wa sasa hasa kwa makundi yenye uhitaji yaliyosahaulika na kukuza ulinzi na usalama kwa mama na mtoto.

Ujumbe huo pamoja na kuwa mzito pia utafanya safari ya kuangalia miradi ya Bunge iliyopewa chapuo na fedha za Umoja wa Mataifa pia watatembelea eneo la dawati la Jinsia Chang'ombe na kutembelea taasisi ya PASADA.

Maeneo mengine ni ghala la Chakula Kizota, miradi ya TASAF na pia kiwanda cha kusindika mafuta kilichopo Dodoma.
Kiongozi wa ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana na wataalam kutoka Mashirika ya Umoja wa Mataifa, Anders Ronquist kutoka Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Sweden (SIDA) akizungumza jambo kwa niaba ya ujumbe huo ulipotembelea wizara hiyo jana 14/11/2016 jijini Dar Es Salaam.
Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akitoa neno la shukrani kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome (kushoto) wakati wa ziara ya ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana na wataalam kutoka Mashirika ya Umoja wa Mataifa ulipotembelea wizara hiyo.
Sehemu ya ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana na wataalam kutoka Mashirika ya Umoja wa Mataifa ulipotembelea Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria jana 14/11/2016 jijini Dar Es Salaam. 

Balozi wa Sweden nchini Mhe. Katarina Rangnitt akizungumza jambo wakati akiagana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome (kushoto). Kushoto ni Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez akiteta jambo na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Amon Mpanju mara baada ya kumalizika kwa mkutano na ujumbe wa Nordic uliotembelea wizara hiyo jana.
Deepika Nath wa UN Women akimwonyesha kitu Edgar Kiliba (kushoto) wa Ofisi ya Mkuu wa Umoja wa Mataifa kitengo cha mawasiliano mara ya kumalizika kwa mkutano wa ujumbe kutoka nchi za Nordic ulioambatana na wataalam kutoka Mashirika ya Umoja wa Mataifa ulipotembelea Wizara ya Mabo ya Katiba na Sheria jana 14/11/2016 jijini Dar es Salaam.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.