ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, October 6, 2016

MCHANGO WA UINGEREZA WAENDELEZA UTOAJI MISAADA KWA WAKIMBIZI NCHINI

Wakimbizi wakigaiwa msaada wa chakula kwenye kambi zao. (Picha zote na Tala Loubieh wa WFP).

Ni kutokana na mchango mkubwa wa Paundi za Uingereza milioni 1 (Dola za Marekani milioni 1.3) kutoka katika Shirika la Misaada la Uingereza (Department for International Development --DFID), kwamba Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) limeweza, walau kwa muda, kusitisha mpango wa kupunguza kiasi cha mgao wa chakula uliopangwa kwa ajili ya wakimbizi nchini Tanzania.
 Wakimbizi wakigaiwa msaada wa chakula kwenye kambi zao. (Picha zote na Tala Loubieh wa WFP).
WFP ilikuwa imepanga kupunguza kiasi cha mgao kuanzia Oktoba kwa karibu robo milioni ya wakimbizi kutokana na kukosekana kwa fedha za kuendeshea shughuli za WFP za kuhudumia wakimbizi nchini Tanzania. Sasa – walau kwa muda huu – shughuli hizi zitaendelea kama kawaida.
“Uingereza inaungana na Umoja wa Mataifa na jumuiya ya kimataifa katika kusaidia ukarimu mkubwa wa Serikali na watu wa Tanzania wa kuwakaribisha wale wanaotafuta usalama kutokana na mapigano nchini Burundi na ukanda wa Maziwa Makuu,” alisema Vel Gnanendran, ambaye ni Mkuu wa DFID. “Kwa hiyo, tunatoa mchango wa nyongeza mara moja wenye thamani ya Paundi milioni 1 ili kuisaidia WFP kuendelea kutoa chakula kwa idadi inayokuwa ya wakimbizi wanaowasili nchini Tanzania. Nyongeza hii inafanya jumla ya mchango wetu kwa WFP kufikia Paundi milioni 6.5 tangu mgogoro huu uanze.”

WFP husambaza chakula kinachookoa maisha kwa wakimbizi wapatao 236,000 wanaoishi katika kambi tatu mkoani Kigoma, kaskazini magharibi mwa Tanzania. Wakimbizi wanategemea msaada huu, ambao ni pamoja na mahindi, kunde, mafuta ya kupikia, chumvi na mchanganyiko wa uji wenye virutubisho.

“WFP inatoa shukrani za dhati kwa DFID kwa mchango wao katika kipindi hiki muhimu,” alisema Michael Dunford, Mwakilishi wa Nchi wa WFP nchini Tanzania. “Wakati ambapo fedha zaidi za nyongeza zinahitajika haraka ili kukidhi mahitaji ya wakimbizi hadi kufikia mwisho wa mwaka huu, tunathamini sana mchango huu mkubwa.”

Licha ya kuhakikisha upatikanaji wa mahitaji ya kikalori ya kila siku ya wakimbizi, WFP hutoa chakula kilichopikwa katika vituo vya mpito na kupokelea wakimbizi na vituo vya afya. Katika kambi za wakimbizi, WFP pia husaidia akina mama wajawazito na wale wanaonyonyesha, na pia watoto wenye utapiamlo wa kiwango cha kati walio na umri wa chini ya miaka mitano kwa kuwapatia unga wenye virutubisho au mchanganyiko wa uji ulioongezewa virutubisho.

Kila siku, mamia ya wakimbizi kutoka Burundi huwasili katika mpaka wa Tanzania, hasa kutokana na kuendelea kwa mapigano nchini mwao. WFP inamudu kutimiza wajibu wake kutokana na misaada itokayo kwa wahisani. Lakini kutokana na kuendelea kumiminika kwa wakimbizi, Shirika lina hali ngumu ya kifedha. Michango isipoongezeka, usalama wa chakula na lishe wa wakimbizi unaweza kuwa katika hatari kubwa.

Ili kuendeleza shughuli za kuwahudumia wakimbizi hadi mwisho wa mwaka, WFP inahitaji Dola za Marekani milioni 7.6. Jumla ya Dola za Marekani milioni 63.6 zinahitajika hadi kufika Agosti, 2017.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.