ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Monday, May 9, 2016

DC WA WILAYA YA SHINYANGA AKABIDHI HATI 92 ZA KIMILA

Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Mhe. Josephine Matiro akimkabidhi Anna Kadilana mkazi wa kijiji cha Nyida hati yake ya hakimiliki ya kimila. Anna alisema, "Nimeamua kukata hakimiliki kwa sababu ya kukwepa usumbufu hasa wa mipaka ambao ulikua unatokea mara kwa mara
Haji Kihwele kutoka shirika la Oxfam akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi hati za hakimiliki za kimila zilizofanyika katika kijiji cha Nyida.
Afisa Mtendaji wa kijiji cha Nyida John Sahani Nungula akizungumza katika hafla hizo; Alitaja shughuli za wakazi wa kijiji chake kuwa wengi ni ukulima, ufugaji na biashara ndogondogo na kwamba mazao yanayolimwa zaidi ni mpunga, mahindi, karanga, kunde, njugu mawe na mihogo
kurugenzi wa SHIDEPHA+ Venance Muzuka akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi hati za hakimiliki za kimila zilizofanyika katika kijiji cha Nyida.
Meneja wa program kutoka shirika la Oxfam Bonaventure Joseph akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi hati za hakimiliki za kimila zilizofanyika katika kijiji cha Nyida. Kulia kwake ni Peppy Sparrow kutoka Oxfam Scotland ambao ndio wafadhili wa mradi huu kupitia serikali ya Scotland.
Wakazi wa kijiji cha Nyida wakihudhuria hafla ya kukabidhi hati za hakimiliki za kimila.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba akizungumza katika hafla hiyo. Kibamba alisema “Kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo; Oxfam na SHIDEPHA+ tumefanikiwa kutekeleza mradi wa kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ndani ya vijiji vinne ambavyo ni Shabuluba, Nyida, Mwenge na Puni. Mradi ulioanza mwezi wa Februari 2016 na sasa upo katika hatua za mwisho za utekelezaji.”
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Kiomoni Kibamba akizungumza katika hafla hiyo. Kibamba alisema “Kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo; Oxfam na SHIDEPHA+ tumefanikiwa kutekeleza mradi wa kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ndani ya vijiji vinne ambavyo ni Shabuluba, Nyida, Mwenge na Puni. Mradi ulioanza mwezi wa Februari 2016 na sasa upo katika hatua za mwisho za utekelezaji.”
Wakazi wa kijiji cha Nyida wakiangalia hati zao walizopokea. 
Anna Kadilana mkazi wa kijiji cha Nyida akionyesha hati yake ya hakimiliki ya kimila. Anna alisema, "Nimeamua kukata hakimiliki kwa sababu ya kukwepa usumbufu hasa wa mipaka ambao ulikua unatokea mara kwa mara"
Wakazi wa kijiji cha Nyida wakihudhuria hafla ya kukabidhi hati za hakimiliki za kimila.
MKUU wa Wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro amekabidhi jumla ya hati za hakimiliki za kimila 92 kwa wakazi wa kijiji cha Nyida mkoani Shinyanga.

Hatua hiyo ya ugawaji wa hati ilifanyika hivi karibuni katika Wilaya hiyo, baada ya viwanja vya wakazi hao kupimwa na kupatiwa mafunzo ya matumizi bora ya ardhi.

Alisema Hati hizo zitawasaidia wananchi kupunguza au kuondoa kabisa migogoro ya ardhi katika wilaya hiyo kwa sababu watakuwa wanamiliki maeneo yao kisheria.

Matiro alisema migogoro mingi ya ardhi inatokea kutokana na watu kutokuwa na hati zinazoonyesha ukubwa wa maeneo yao na kusababisha mgogoro baina ya mtu na mtu.

Matiro aliwapongeza maafisa ardhi kwa kuweza kufanya kazi hiyo kwa kutumia shilingi milioni tatu kwa kila kijiji tofauti na milioni tisa iliyoelekezwa na serikali.

“Natoa shukrani zangu za dhati  kwa ushirikiano mkubwa na ufadhili kutoka kwa wadau wa maendeleo ikiwemo Shirika la Oxfam na SHIDEPHA+ kwa kusaidia kutoa mafunzo ya matumizi bora ya ardhi ili wananchi wa wilaya yangu kufahamu umuhimu wa hati hizo,” alisema.

Kwa Upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, Kiomoni Kibamba alisema kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo Oxfam na SHIDEPHA+ wamefanikiwa kutekeleza mradi wa kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ndani ya vijiji vinne ambavyo ni Shabuluba, Nyida, Mwenge na Puni.

Alisema mradi huo ulianza mwezi wa Februari 2016 na sasa upo katika hatua za mwisho za utekelezaji katika vijiji hivyo.

Alitaja changamoto mbalimbali  za kupata haki miliki za kimila kuwa ni pamoja na ukosefu wa rasilimali fedha ndani ya jamii, baadhi ya wananchi kugubikwa na umaskini na kukosa fedha kwa ajili ya kuchangia gharama za upimaji.

Kibamba alisema changamoto nyingine ni pamoja na kukosekana kwa vigezo elekezi vya Wizara na kanuni ya sheria ya ardhi ya vijiji ya mwaka 1999 kuhusu kupatiwa hati miliki ndani ya serikali za vijiji ambavyo ni pamoja na kukosa ofisi zenye hadhi za Halmashari za vijiji pamoja na ukosefu wa masijala za ardhi na daftari za ardhi za vijiji kwa ajili ya usajili wa Hakimiliki za kimila.

“Faida zilizotokana na mradi wa kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi katika halmashauri ni pamoja na uhamasishaji na utoaji wa elimu juu ya hati za haki miliki za kimila uliotolewa kwa vijiji vinne pamoja na kupunguza na kutokomeza kabisa migogoro ya ardhi ndani ya jamii katika vijiji husika,” alisema Kibamba.

Alitaja faida nyingine kuwa ni pamoja na utunzaji wa mazingira kwa kupanga matumizi sahihi ya ardhi ndani ya mipaka ya kijiji, umiliki wa ardhi kisheria ndani ya jamii kwa wananchi kupatiwa hati za hakimiliki za kimila pamoja na jamii kupata uwezesho wa kifedha kutoka taasisi za kifedha baada ya kupatiwa hati miliki.

Nae miongoni mwa wakazi waliopokea hati hizo ambae ni  Mkazi wa Kijiji cha Nyida, Flora Nkingwa alishukuru kukabidhiwa hati hizo kwani sasa anamiliki eneo lake kisheria.

Nkingwa alisema eneo alilopatiwa hati lina ukubwa wa nusu ekari ambalo analitumia kwa kilimo cha Mahindi na Karanga.

Hati hizo za bila kikomo zilitolewa kwa mchanganuo wa hati 75 za familia, hati 7 za wanawake, hati 5 za wanaume, hati 2 za Taasisi na hati 3 za ukoo.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.