ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, March 15, 2013

HII HAPA VIDEO ILIYOMUWEKA MATATANI MKUU WA USALAMA CHADEMA



Lwakatare alikamatwa juzi makao makuu ya chama hicho na kupelekwa katika Makao Makuu ya Polisi kwa mahojiano.

Bakari Kiango na Nuzulack Dausen, MWANANCHI
Polisi wamezidi kumbana Mkuu wa Usalama wa Chadema, Wilfred Lwakatare baada ya kupekua nyumbani kwake kwa siku ya pili mfululizo.

Lwakatare, ambaye ni mbunge wa zamani wa Jimbo la Bukoba Mjini kupitia CUF, alikamatwa juzi mchana kwa kutuhumiwa kwa kufanya uchochezi wa uvunjifu wa amani baada ya kunaswa kwenye picha ya video iliyorushwa kwenye mitandao ya kijamii.

Upekuzi wa pili
Nyaronyo Kicheere, ambaye ni Mwanasheria wa Lwakatare, aliliambia gazeti hili jana kuwa mteja wake, ambaye anashikiliwa na polisi hao, alipelekwa nyumbani kwake Kimara-King’ong’o jijini Dar es Salaam kwa ajili ya upekuzi huo.

Ilikuwa mara ya pili kwa Lwakatare kupekuliwa kwani mara ya kwanza ilikuwa juzi jioni baada ya kuhojiwa Makao Makuu ya Jeshi la Polisi. Lwakatare, ambaye alitolewa Kituo cha Kati cha Polisi, alipelekwa jana kwa msafara wa magari mawili ya polisi chini ya ulinzi mkali.

Nyaronyo alisema kuwa msafara huo uliondoka saa 10.00 jioni kwa ajili ya safari hiyo ya Kimara wakitokea katikati ya Jiji la Dar es Salaam kilipo Kituo cha Kati cha Polisi. Alisema kuwa uamuzi huo ulifikiwa baada ya kikao kizito kati ya maofisa wa Idara ya Upelelezi (DCI) na wale wa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP).
“Hawa watu walikuwa na kikao kirefu siku nzima ya leo (jana) nadhani walikuwa wanaangalia kama kuna uwezekano wa kumshtaki au la mteja wangu.Walipomaliza kikao waliamua turudi tena nyumbani kwa Lwakatare ili kuendelea na upekuzi,” alieleza Kicheere.

Kama ilivyokuwa juzi, upekuzi kwa Lwakatare uliongozwa na Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Obadia Jonas.

Polisi wanasemaje
Msemaji wa Polisi, Advera Senso alisema kuwa bado wanaendelea kumshikilia Lwakatare huku wakiendelea na uchunguzi wa suala hilo. “Kama kukiwa na taarifa za ziada nitawajulisha msiwe na wasiwasi,” alisema Senso na kukata simu.

Lwakatare alikamatwa juzi saa saba mchana katika makao makuu ya chama hicho na kupelekwa katika Makao Makuu ya Polisi kwa mahojiano.

Juzi siku nzima mitandao ya kijamii ilikuwa imetawala na habari picha ya video ikimwonyesha Lwakatare akidaiwa kupanga mikakati ya kumteka Mhariri Mtendaji wa Mwananchi, Dennis Msacky kwa madai kuwa anashirikiana na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, kutengeneza migogoro.
Pia, Lwakatare alionekana akitoa maelekezo kwa watu , ambao sura zao hazikuonekana, akiwataka kufuatilia nyendo za Msacky.

Chadema wapinga
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema mkanda wa video unaoonyeshwa kwenye mitandao ya kijamii ukimwonyesha Lwakatare akipanga njama za uhalifu hauna uhalisia na kwamba huo ni uzushi ulioratibiwa na kufanikishwa na vyombo vya dola.
Pia Dk Slaa alidai kuna mpango mwingine kabambe unaofanywa na idara za dola kuhakikisha kuwa Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa anakamatwa kutokana na sumu anazotema bungeni na kwingineko dhidi ya Serikali.

Dk Slaa alisema kuwa taarifa za kuwapo njama za kukichafua chama chake kupitia mkanda huo wa video alizipata kutoka ndani ya Serikali Jumatatu iliyopita hata hivyo, wakati akiendelea kupanga mkakati wa kushughulikia tayari ulikuwa umeshaingizwa katika mitandao ya kijamii.

Tupe maoni yako

1 comments:

  1. dah ebwana na chadema ichunguzwe vizuri am sure huyu hajifanyii haya kuna watu nyuma yake

    ReplyDelete

Note: Only a member of this blog may post a comment.