ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, May 26, 2011

LISSU NA WENZAKE MARUFUKU NYAMONGO

Tundu Lissu akionyesha shati lake analodai kuchaniwa na polisi baada ya kumpa kichapo akiwa nje ya Mahakama ya Wilaya ya Tarime, baada ya kupata dhamana jana. Picha na Anthony Mayunga

Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu, ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Katiba na Sheria, na wenzake saba ambao juzi walifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Tarime na kusomewa mashtaka matatu ya kuingia eneo la hospitali bila kibali, kufanya mkutano na kuzuia watu kufanya kazi, wamepata dhamana lakini wamezuiwa kutembelea maeneo ya Nyamongo hadi kesi inayowakabili itakapokwisha.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya wilaya hiyo, Yusto Roboroga alitoa uamuzi huo akisema ni kwa mujibu wa kifungu cha Sheria Namba 148 cha Makosa ya Jinai, kilichofanyiwa marekebisho mwaka 2002, ambacho kinatoa haki kwa watuhumiwa kupata dhamana. Alitoa uamuzi huo baada ya kupitia pingamizi lililowekwa na upande wa mashtaka kutaka wasipewe dhamana. Hata hivyo, alisema: “Washtakiwa wanazuiwa kutembelea maeneo ya Nyamongo mpaka kesi hiyo itakapokuwa imekwisha."

Hakimu Ruboroga alitaja masharti ya dhamana hiyo kuwa ni kusaini mkataba wa dhamana wa Sh5 milioni kwa wadhamini wawili wanaoaminika. Kwa wasio wakazi wa Tarime, alisema watatakiwa kupeleka mahakamani hati za mali isiyohamishika. Washtakiwa wote walikidhi masharti na kuachiwa kwa dhamana hadi Juni 26, mwaka huu kesi hiyo itakapotajwa tena.

Juzi, Lissu na wenzake, Waitara Mwita Mwikwabe, Stanslaus Nyembea, Anderson Deogratias Chacha, Andrew Andalu Nyandu, Mwita Marwa Maswi, Bashiri Abdalllah Selemani na Ibrahimu Juma Kimu walifikishwa mbele ya mahakama hiyo na kusomewa mashtaka hayo matatu na Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Casmir Kiria ambaye alisema, waliyatenda Mei 23, majira ya saa nne usiku. Wote walikana mashtaka hayo.


Hisani ya gazeti la Mwananchi

Tupe maoni yako

1 comments:

  1. Ina maana Tindu Lisu na wana chadema wanautindio wa akili mpk kufikishwa hapa walikuwa wanatettetea Watanzania wa Nyamongo au Wana Nyamongo wanaupungufu wa akili au Ni Polisi wanyamogo wako sawa kuzitupa maiti kam mfuko mchafu maana walikiri hilo au Barrick kutotambua mauaji na hizo maiti mpk inafikia Barick wanasema hawana habari na maiti kutupwa!!!! Je, Barrick wanawasaidia wananchi wa Nyamongo? Wamewajengea barabara, zahanati, shule? Wametoa scholarships ili vijana wasome sekondari, Chuo Kikuu? Au kazi kuiba dhahabu yetu? Watu wamepoteza maisha shauri ya vimawe vyenye chembe chembe za dhahabu! Mzungu kwa dhahabu, almasi, Tanzanite! Yaani! Je, Barrick watawasaidia wafiwa, mfano huyo mjane mwenye mimba?

    ReplyDelete

Note: Only a member of this blog may post a comment.