ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, August 17, 2010

TUME YA UCHAGUZI YAKATAA KUTOA FOMU YA KUGOMBEA URAIS KWA CHAMA CHA SAU.

Tume ya uchaguzi Zanzibar imekataa kutoa fomu za kuwania urais wa Zanzibar kwa chama cha SAU kutokana na kujitokeza wagombea wawili wanaowania nafasi hiyo kupitia chama kimoja.

Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar Salim Kasim amesema wagombea hao waliojitokeza kuchukua fomu ni Haji Ramadhani Haji barua yake iliwasilishwa Ogasti 12 na Haji Musa Kitole barua yake iliwasilishwa Agosti 13.

Amesema kwa mujibu wa sheria za uchaguzi kila chama kitalazimika kuteuwa mgombea mmoja kushiriki katika uchaguzi huo, hivyo tume imeshindwa kutoa fomu kwa wagombea wa urais kupitia chama hicho.

Hata hivyo mkurugenzi huyo amesema fomu hizo zinaweza kutolewa kwa chama hicho endapo kitawasilisha barua ya kufuta jina moja kati ya wagombea hao wawili

Haji Mussa Kitole na Haji Ramadhan Haji wote kutoka chama cha SAU wakiwa na barua tofauti wakati kitole akiwa na barua ya Mwenyekiti, Ramdhan alikuja na barua kutoka kwa Katibu Mkuu wa chama hicho wote wakidai kupitishwa na chama chao.

Mkurugenzi wa tume ya uchaguzi Zanzibar, Salim Kassim Ali aliwaambia waandishi wa habari kwamba haiwezekani kutolewa fomu mbili kwa chama kimoja kwa kuwa sheria za uchaguzi zimeeleza mgombea mmoja kutoka chama husika ndie anayepaswa kupewa fomu na sio zaidi ya hapo.

Hata hivyo wagombea hao walikuwa na maoni tofauti huku kila mmoja akijitetea kwamba ameteuliwa kihalali na chama chake na kutaka mwenzake arudi katika chama ili kupata ridhaa ya mkutano mkuu ambao ndio wenye maamuzi ya mwisho.

Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) Khatib Mwinyichande aliwataka wagombea wote waliopewa fomu za urais kutimiza masharti yaliowekwa katika ujazaji wa fomu hizo ikiwa pamoja na kurejesha kabla ya Agosti 30 mwaka huu zikiambianishwa na dhamana wa shilingi millioni mbili na wadhamini wasiopungua 200 katika mikoa mitano ya Unguja na Pemba.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.